Kenya Socialist Web Site



October 12  2003

Iraq Imemtumbukia Nyongo Bush

 

Na Ben Barka

 

Mjini Baghdad kuna kaburi la jemadari wa majeshi ya Kiingereza yaliyovamia Iraq. Huyo ni

Jenerali Sir Stanley Maude aliyeuawa wakati wa mashambulizi hayo. Maandishi juu ya kaburi hilo yanamnukuu akisema “tulikuja hapa siyo kama wavamizi bali kama wakombozi.” Hii si hadithi ya

mwaka 2003 bali ni 1917. Wakati huo “wakombozi” hao walioongozwa na Maude waliwaua raia

10,000 wa Iraq kwa kutumia silaha za kemikali. Huo ndio “ukombozi” wa Iraq wa mwaka 1917

 

Iraq kwa hiyo ina historia ndefu ya kuvamiwa na majeshi ya kigeni. Bush (mkubwa na mdogo) hawakuwa wa kwanza

kuvamia nchi hiyo.

 

Mwaka huu majeshi ya Marekani na Uingereza yalipoivamia Iraq (kinyume cha sheria za kimataifa) waliwaua zaidi ya raia

10,000 na askari 20,000. Hii ndiyo gharama waliyolipa Wairaq ili “wakombolewe” na majeshi ya uvamizi.

Vyombo vya habari vimekaa kimya kuhusu gharama hii.

 

Ni tofauti na watu 3000 waliouawa katika ushambulizi wa New York tarehe 9 Septemba 2001. Wakati huo televisheni

zao zilikuwa zikirudia habari hizo usiku na mchana. Lakini hatuambiwi chochote kuhusu halaiki ya Wairaq waliouawa

kutokana na silaha za maangamizi za Marekani.

 

Yale mabomu ya kutawanya (cluster bombs) utayaitaje kama si ya mangamizi. Ndizo zilizowauwa maelfu ya watoto,

wazee  na wanawake nchini Iraq. Habari hizo zilifichwa na badala yake tukawa tunaonyeshwa usiku na mchana mamia

ya raia waliokuwa wakishangilia kuangushwa kwa sanamu ya Saddam.

 

Kuna habari nyingine ambazo zinafichwa. Hatuambiwi kwa nini baada ya “ukombozi” ulioshangiliwa na wananchi wa Iraq

majeshi ya uvamizi yanaendelea kuuawa. Wangapi tunajua kuwa tangu Iraq “ikombolewe” na tangu Bush atangaze ushindi

mnamo Mei majeshi yake yamekuwa yakifa zaidi kuliko wakati wa ushambulizi wenyewe.

 

Badala yake tunaambiwa kuwa bado kuna wafuasi wachache wa chama cha Baath ambao wanaleta ukorofi.  Kama ni

hivyo basi wale Washia wa kusini nao pia sasa wamejiunga na chama cha Baath?

 

Hawatuambii ukweli kuwa Wairaq wa sehemu zote, Shia na Sunni, sasa wanapinga kwa nguvu uvamiaji na utawala wa

Marekani uliopewa jina bandia la utawala wa muungano. Hata hiyo serikali iliyoteuliwa na Marekani inakataliwa na wananchi

kwa sababu ni serikali bandia ya vikaragosi. Ndiyo maana baadhi yao wamelazimika kujiuzulu na wengine wameuawa.

 

Ndiyo maana haipiti hata siku moja bila ya majeshi ya uvamizi kushambuliwa nchini Iraq. Habari hizi hupewa umuhimu

mdogo na badala yake magazeti na TV zimekuwa zikirudia propaganda za Bush

 

Naye Bush anaendelea kutuambia kuwa kuna wakorofi wachache tu ambao wanapinga demokrasia na mageuzi. Ukweli

ni kuwa “wakorofi” hawa ndiyo wanaomtia kiwewe na kumfanya akimbilie Umoja wa Mataifa na kuomba msaada wa

majeshi ya kimataifa.

 

Na vyombo vya habari vinaendelea kumkariri Bush bila ya maswali. Vinatumika kama vyombo vya kuwapumbaza raia wa

Marekani. Matokeo yake ni kuwa raia wa kawaida wa Marekani anaamini kuwa Saddam ndiye aliyepanga uvamizi wa New

York mnamo 2001, kuwa yeye amekuwa akishirikiana  na Osama bin Laden na Al Qaida.

 

Raia huyu wa kawaida anaamini kuwa Saddam alikuwa tishio kubwa kwa usalama wa Marekani. Hizi ni nguvu za vyombo

vya habari katika kuwapumbaza raia. Wanaokataa kupumbazwa huitwa wahaini na maadui wa taifa. Wengi wao wamefungwa

bila ya kuhukumiwa au kufunguliwa mashtaka. Huo ndio uwezo uliopewa serikali ya Bush katika nchi hii inayojiita ya

demokrasia na utawala wa sheria.

 

Ni watu wachache tu kama akina Profesa Chomsky, John Pilger na Edward Said (marehemu) ambao wamekuwa msitari wa

mbele katika kuandika waziwazi wakifichua ukweli.

 

Wamekuwa wakionyesha kuwa Marekani ni nchi ya kibeberu ambayo ina historia ndefu ya kuzivamia nchi za ulimwengu wa

tatu na kupora utajiri wake. Uvamizi huu wa Iraq ni wa 73. Historia hii ya uvamizi inaanzia pale wazawa wa Marekani

walipouawa na kuporwa nchi yao. Wazawa wachache waliobaki wamewekwa katika mbuga za maonyesho kwa ajili ya watalii.

 

Na kila uvamizi unapofanyika basi kazi ya serikali huwa ni kuwapumbaza wananchi kwa kuficha ukweli. Marekani ilipotaka

kushambulia utawala wa Spain huko Amerika ya kusini walianza kwa kusingizia kuwa Spain ilikuwa imezamisha meli ya

Marekani iitwayo Maine. Baada ya hapo magazeti yakarudia uwongo huu na wananchi wakatayarishwa kwa mashambulizi.

 

Halafu mnamo miaka ya 1960 Marekani ilieneza uwongo mwengine kuwa Umoja wa Kisovieti (USSR) ulikuwa ukiunda

makombora makubwa yaliyokuwa yameelekezwa Marekani. Waandishi wakapewa nyaraka bandia nao wakaeneza uwongo

mkubwa ili kuwatayarisha wananchi kwa matumizi ya mabilioni kwa kuunda silaha za kisasa ili kukabiliana na “tishio la

kikomunisti.”

 

Marekani walipotaka kuivamia Jamhuri ya Kisosashilisti ya Vietnam walianza kwa kueneza uwongo kuwa nchi hiyo ilikuwa

imeshambulia manowari mbili za Marekani katika Ghuba ya Tonkin. Magazeti yakarudia mara kwa mara uwongo huu na

wananchi wakapandisha mori wakimtaka Rais Johnson aishambulie Vietnam.

 

Mnamo miaka ya 1980 Rais Reagan alibuni visingizio vya kuwashambulia wananchi wa Amerika ya Kusini waliokuwa

wakipigana dhidi ya madikteta vibaraka wa Marekani. Mfano mmoja ni nchi ndogo ya Nicaragua ambako wanaukombozi

wa Sandinista wakiongozwa na Daniel Ortega waliiangusha serikali dhalimu ya Somoza iliyokuwa ikiungwa mkono na

Marekani.

 

Marekani ikabuni uwongo kuwa Sandinista walikuwa ni tishio kwa Marekani. Ndipo Reagan alipowakusanya vibaraka

magaidi waitwao Contra na kuwapa silaha na fedha ili kupindua utawala wa Sandinista. Matokeo ya ugaidi huu wa Reagan

ni wananchi 70,000 kupoteza maisha yao huko Nicaragua.

 

Na hayo si ya Reagan tu. Leo hii utawala wa Geroge W Bush unaendelea kutoa hifadhi kwa wauaji, watesaji, wateka nyara

ndege na magaidi kutoka Cuba na kwengineko. Magaidi zaidi wanaendelea kutayarishwa na kupewa mafunzo katika shule

 maalum iliyopo Fort Benning (Georgia).

 

Halafu Bush anadai kuwa anapigana na ugaidi duniani. Naye anaungwa mkono na propaganda zinazoendeshwa na tajiri

mkubwa Rupert Murdoch anayemiliki mtandao wa magazeti na TV kama Fox. Idhaa hii kazi yake kubwa imekuwa ni

kumpigia vigelegele Bush na kuwapumbaza wananchi.

 

Hali hii ya upigaji debe itaenelea kuwa mbaya. Kwani hivi sasa tume ya utangazaji huko Marekani inaongozwa na Michael

ambaye ni mtoto wa waziri wa mambo ya nje Colin Powel. Tume hii inakusudia kubadili sheria ili kuruhusu makampuni

machache yaweze kuhodhi vyombo vya habari.

 

Matokeo yake ni kuwa Fox pamoja na makampuni mengine manne yatakuwa yanadhibiti asilimia 90 ya TV za kitaifa nchini

Marekani. Huo eti ndio uhuru wa habari.

 

Licha ya TV njia nyingine kubwa ya kueneza propaganda ni Internet. Hivi sasa asilima 60 ya mitandao hii inatawaliwa na

makapuni 14 kama Fox, Disney, AOL na Time Warner. Hapa pia tunaona jinsi Internet inavyohodhiwa na akina Murdoch.

 

Hao ndio watakaoamua aina ya habari zitakazoenezwa. Huo uhuru wa habari tunaoupigia kelele haupo chini ya utandawazi

na ubeberu. Ni ndoto ya mchana. Ndiyo maana ukweli huwa unafichwa na uwongo huenezwa.

 

Kwa mfano ni wangapi kati yetu tunaelewa kuwa uvamizi na uporaji huu wa Iraq ni uvamizi wa 73 katika historia ya ubeberu

wa Marekani. Ukiachia haya mashambulizi ya waziwazi kuna oparesheni za siri zaidi ya 100 dhidi ya mataifa ya kigeni.

 

Kuanzia mbinu za kuwaangusha akina Mohammed Mosadeq wa Iran na Salvador Alliende wa Chile hadi majaribio ya

kumuua Rais Fidel Castro, ubeberu wa Kimarekani umekuwa daima ukitumia silaha kuzikandamiza nchi za dunia ya tatu.

Hiyo ni khulka ya ubeberu iliyokuwepo tangu karne na karne.

 

Vyombo vya habari vya magharibi vimekuwa vikificha ukweli huu. Kama vile Iraq iliposingiziwa kuwa inahatarisha usalama

wa dunia. Mfano mwengine ni pale Marekani ilipodanganya ulimwengu kuwa Spain ilikuwa imeshambulia manowari ya

Kimarekani iitwayo Maine. Ndipo Marekani ilipotumia kisingizio cha kuishambulia Spain.

 

Pia mnamo 1960 waandishi walipewa nyaraka za uwongo zikionyesha kuwa eti Umoja wa Sovieti (USSR) ulikuwa unaunda

makombora yenye uwezo mkubwa kushinda Marekani. Ndipo Marekani ilipopata kisingizio cha kuunda silaha kubwa ili

kukabiliana na hilo “tishio” la Kisovieti.  Uwongo huu ulienezwa na waandishi bila ya kudadisi.

 

Ni kama vile walivyoeneza uwongo kuwa wanaharakati wa Vietnam walikuwa wamezamisha manowari mbili za Marekani

katika ghuba ya Tonkin. Hawakudai kuonyeshwa ushahidi wala hawakudadisi. Badala yake tahariri zilicharuka kutaka

Vietnam nayo ishambuliwe.

 

Wimbo huo ndio aliokuwa akiutaka Rais Johnson ambaye aliutumia kama kisingizio cha kuishambulia Vietnam kwa mabomu

ya sumu na silaha nyingine za maangamizi. Kwani Marekani ni wamiliki na watumaiaji wakubwa wa silaha za maangamizi.

Haya hayasemwi na vyombo vya propaganda.

 

Na hivi karibuni tumeona jinsi Rais Bush na Waziri Mkuu Tony Blair walivyobuni uwongo na jinsi walivyowadanganya raia

wao kabla ya kuishambulia Iraq.  Uchunguzi wa Jaji Hutton huko London hivi sasa unaonyesha kiasi gani unafiki na uzandiki

ulivyokuwa ukitawala propaganda za kivita.

 

Mengi zaidi yatafichuka wakati wananchi wa Marekani nao watakapofanikiwa kuwa na uchunguzi wao. Hizi zitakuwa ni

skandali kubwa kushinda zile za Watergate.

 

Colin Powell alidiriki kusimama mbele ya Baraza la Usalama (UN) na kutoa vielelezo vya uhange na picha za kubuni akidai

eti alikuwa na uhakika Saddam alimiliki silaha za maangamizi. Alipoambiwa tumuachie basi Bw Blitz na wataalamu wenzake

waendelee na uchunguzi wao huko Iraq akasema Blitz anaregarega mno.

 

Leo hii Marekani baada ya kuivamia Iraq imeshindwa kufichua hizo silaha za maangamizi kwa kisingizio eti Saddam alikuwa

mjanja na huenda amezificha mahali pasipojulikana. Kama ni hivyo basi mbona wakati ule Marekani ilijifanya ilikuwa na

uhakika kuwa inajua zilipo silaha hizo? Kama Saddam alikuwa na hizo silaha iweje akubali kupinduliwa bila ya kuzitumia?

Aliziunda kama pambo tu?

 

Ukweli ni kuwa walitudanganya. Tarehe 9 July Donald Rumsfeld alipoulizwa alitabasamu na kusema kuwa Marekani kamwe

haikuwa na ushahidi wa kutosha. Aliungwa mkono na naibu wake  Paul Wolfowitz ambaye alisema kuwa silaha za

maangamizi ni sababu pekee ya kuwafanya watu waunge mkono uvamizi wa Iraq.

 

Sasa hata Bush anaungama kuwa hakukuwa na ushahidi wowote kuwa Saddam alihusika kwa njia yeyote na mashambulizi

ya New York ya 2001. Hata hivyo gazeti moja linaripoti kuwa asilimia 69 ya Wamarekani wanagali wanaendelea kuamini

kuwa Saddam alihusika. Inaonyesha jinsi kasumba inavyofanya kazi huko Marekani.

 

Tarehe 11 Septemba kila mwaka serikali ya Marekani huwakumbuka watu 3000 waliokufa kule New York. Wakati huohuo

zaidi ya raia 10,000 wamekufa nchini Iraq kutoka na uvamizi wa Marekani. Hawa hawakumbukwi.  Malaki ya wananchi

wa Iraq  pia wamekufa katika muda wa miaka 12 kutokana na vikwazo vya uchumi. Hawa hawakumbukwi.

 

Wakati huohuo hali inazidi kuwa mbaya kwa majeshi ya Marekani huko Iraq. Kwa mujibu wa gazeti la New York Times

la tarehe 22 Septemba jumla ya askari wa Marekani 304 wamekufa tangu kuanza kwa uvamizi. Likinukuu ripoti ya Pentagon

gazeti hilo linasema tangu Bush kutangaza ushindi tarehe 1 Mei zaidi wa askari 165 wamekufa. Zaidi ya 1100 wamejeruhiwa

vibaya.

 

Katuni iliyochorwa katika gazeti moja huko Marekani inaonyesha makaburi maalum ya wale askari waliokufa wakati wa

kuivamia Iraq. Lakini ubavuni kuna makaburi ya wale askari wanaoendelea kufa baada ya kumalizika kwa vita vya uvamizi.

 

Haya makaburi ya pili yamefurika na nafasi sasa haitoshi. Kwani kila siku idadi ya askari wa Marekani wanaendelea

kushambuliwa na kufa huko Iraq. Mimi sijaona TV za magharibi zikionyesha maiti hizi zikirudishwa nyumbani na kuzikwa.

 

Msemaji wa majeshi ya Marekani, Luteni Kanali George Krivo, alisema kuwa kila siku majeshi yake huko Iraq

yanashambuliwa mara kumi hadi ishirini. Alisema, “tutaendelea kushambuliwa, mashabulizi haya yanazidi kuwa ya hali ya juu.”

 

Bush na Blair walipokuwa wakijiandaa kuivamia Iraq wapelezezi na majasusi waliwatahadharisha kuwa kwa kufanya

hivyo tishio la ugaidi dunianai lingeongezeka. Huko Uingereza kuna kamati ya usalama iitwayo Intelligence and Security

Committee (ISC) inayoongozwa na mbunge wa chama cha Labour aitwaye  Ann Taylor.

 

Kamati hii ilitoa onyo hili na kusema kuwa serikali ilikuwa inawadanganya wananchi. Kamati ilimwambia Blair kuwa

hakukuwa na ushahidi wowote kuwa Sadam na Osama walikuwa wakishirikiana. Pia ISC ilisema kuwa si kweli kama

alivyosema Blair kuwa Saddam alikuwa na silaha za maangamizi ambazo zinegeweza kushambulia nchi za magharibi katika

muda wa dakika 45 tu.

 

Pia huko Uingereza kuna kamati ya ya pamoja ya mashirika ya ujasusi iitwayo Joint Intelligence Committee (JIC).  Hii

inaunganisha majasusi kutoka MI6, MI5, GCHQ, Defence Intelligence na kadhalika. Tarehe 10 February mwaka huu JIC

ilimuonya Blair kuwa kuishambulia Iraq kutaongeza ugaidi na wakasema kuwa Saddam hakuwa tishio kwa usalama.

 

Blair badala ya kusikiliza ushauri huu wa wapelelezi aliendelea kuwahadaa umma. Licha ya habari hizi za JIC na ISC Tony

Blair aliliambia bunge tarehe 18 Machi kuwa Saddam alikuwa anahatarisha usalama wa ulimwengu kutokana na silaha zake

za maangamizi.

 

Ingawa kulikuwa na upinzani mkubwa, wengi wa wabunge walidanganyika na kumuunga mkono Blair. Sasa baada ya siri

hizi ya ISC na JIC kuwekwa wazi Bw Blair ameachwa kwenye mataa. Tayari uchaguzi mdogo wa Brent East hivi majuzi

umeonyesha kuwa chama cha Labour kimeanza kuporomoka, kwani kimepoteza kiti kilichokuwa kinashikilia kwa muda mrefu.

 

Tarehe 1 Mei Rais Bush alitangaza kuwa vita vya kumg’oa Saddam vilimalizika. Ilikuwa ni sherehe kubwa. Lakini kama

ilivyotabiriwa na wapepelezi, huo haukuwa mwisho wa mapigano. Kwa kweli tunaweza kusema vita ndio kwanza vimepamba

moto.

 

Kama tulivyona, majeshi ya Marekani yanashambuliwa karibu mara ishirini kila siku. Na haipiti siku bila ya askari wa

Marekani kuawa. Siku hizi TV zao hata hazionyeshi habari hizi. Kwa mfano BBC inatanguliza habari za mkutano wa IMF

huko Dubai. Habari inayofuata ni ile ya kuuawa kwa askari wawili wa Marekani na kujeruhiwa 13 nchini Iraq.

 

Marekani ina askari 140,000 huko nao wanajiuliza lini watarudi nyumbani. Rumsfeld alipowatembelea aliulizwa suala hilo

naye akajibu kuwa itabidi waendelee kukaa huko na kuhimili mashambulizi ya Wairaq.

 

Inasemekana ili kudhibiti mashambulizi haya ni lazima kuwa na angalao majeshi 500,000. Ndivyo walivyofanya huko

Vietnam na mwishowe wakalazimika kufyata mkia na kukimbia.

 

Lakini suala ni kuwa watapata wapi askari laki tano. Siyo tu askari hao hawatakubali kwenda huko bali gharama itakuwa

ni kubwa mno. Bush anajaribu kuzishawishi nchi zingine zipeleke majeshi yao. Labda akina Museveni wanaweza kuwapeleka

askari wao. Mtumikie kafiri upate mradi wako ndiyo sera ya Museveni na wenzake.

 

Lakini Bush anachotaka ni kuungwa mkono na mataifa makubwa  kama Ufaransa au Ujerumani. Nao wamesema kuwa

hawataunga mkono mpaka Iraq ikabidhiwe kwa Umoja wa Mataifa. Bush naye hakubali kuachia ngawira ya Iraq. Labda

atakachofanya Bush ni kuunda jeshi la Wairaq wenyewe. Lakini majeshi haya ya vibaraka hayatakuwa na usalama.

Wananchi wanataka Wamarekani waachie madaraka na waondoke.

 

Huenda ikawa kama ilivyokuwa Vietnam. Huko Vietnam waliunda majeshi ya vibaraka ambao walishambuliwa vibaya na

majeshi ya kizalendo. Na ndipo ikabidi kutuma majeshi ya Marekani “kuwasaidia.” Nao pia walishindwa kukabiliana na

majeshi ya ukombozi.

 

Halafu kuna gharama kubwa ya vita inayoelemea wananchi wa Marekani. Hivi sasa Marekani inatumia $ 2 bilioni kila mwezi

huko Iraq.  Tangu kuanza mashambulizi zimekwishatumika $ 70 bilioni. Bado Bush anahitaji fedha nyingine $ 87 bilioni.

 

Uvamizi wa Iraq utakuwa umewagharimu wananchi wa Marekani karibu $ 160 bilioni. Huo ni mzigo mkubwa. Katika historia

ya Marekani haijawahi kutumia kiasi kama hiki cha fedha katika nchi yeyote ya kigeni. Mara ya mwisho baba yake Bush

aliposhambulia Iraq mnamo 1991 alitumia $ 9 billioni.

 

Sasa kwa kumwaga fedha zote hizo katika uvamizi wa Iraq Bush atakuwa ameongeza nakisi ya bajeti ya serikali yake kwa

aidi ya dola nusu trilioni. Yaani bajeti ya Bush itakuwa na upungufu wa $ 500,000,000,000.

 

Si ajabu chama cha Democrat kimeanza kumshambulia Bush kuwa anatumia fedha nyingi zaidi huko Iraq kuliko matumizi

ya elimu na matibabu nchini Marekani. Ni hao hao Democrats waliokuwa wakipeperusha bendera ya Marekani na

kumuunga mkono Bush sasa wanampinga.

 

Ndiyo kampeni ya urais hiyo. Mwakani Bush itabidi agombee tena na tayari kura za maoni zinaonyesha kuwa watu walio

wengi wamemchoka. Hata Blair naye aliyeungwa mkono na wabunge wengi sasa anaonekana ni mzigo kwa chama cha

Labour. Katika mkutano mkuu wa chama hicho wajumbe walikatazwa kuzungumzia suala la Iraq.

 

Wengi wanatabiri kuwa ushambulizi wa Iraq matokeo yake ni kuanguka kwa Bush na Blair.

 

Uvamizi wa Iraq umewatumbukia nyongo Bush na Blair. Kwa ripoti nyingine iliyotolewa hivi karibuni inasema kuwa hakuna

ushahidi kuwa Iraq ilikuwa na silaha za maangamizi.

 

Kikundi cha watu 1400 kikiongozwa na CIA kitwacho Iraq Survey Group (ISG) kimekuwa kifanya utafiti huko kwa muda

wa miezi sita. Ripoti yake imewasilishwa kwa Bush na Blair. ISG inakanusha ripoti ya National Intelligence Estimate (NIE)

ya Oktoba 2002 iliyodai kuwa Saddam alikuwa akimiliki mamia ya tani ya silaha za sumu.

 

Profesa Richard Stoll wa Chuo Kikuu cha Rice huko Marekani alisema:

 

“Ukiwakamata au kuwaua wapiganaji 1000 wa Al Qaeda haimaanishi kuwa kikundi hicho kimedhoofika kwa kupungua

idadi yao. Ukweli ni kuwa kutokana na uvamizi wa Iraq tunashuhudia kikundi hiki kikizidi kuungwa mkono na vijana wengi

wanaotaka kujiunga nacho.”

 

Hivyo ndiyo historia itakavomkumbuka Bush. Johnson aliangushwa na Vietnam, Bush ataangushwa na Iraq.

 


Published by Kenya Socialist Democratic Alliance (KSDA)
email: harakatips@hotmail.com


Home